Sunday, June 15, 2014

MCHUNGAJI MATATANI KWA KUTOKOMEA NA RAMBIRAMBI ZA ASKOFU MOSES KULOLA

Mchungaji wa Kanisa la Evangelist Assemblies Of God City Centre jijini hapa, Michael Kulola.

MH! Mchungaji wa Kanisa la Evangelist Assemblies Of God City Centre jijini Mwanza, Michael Kulola ametiwa mbaroni kisha kufikishwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkoa wa Mwanza kisa wizi wa fedha za rambirambi za Askofu Moses Kulola kiasi cha Sh. milioni 33.

 
Picha ya marehemu Askofu Moses Kulola enzi za uhai wake.

 Habari zilidai kuwa baada ya kuwekwa nyuma ya nondo, mchungaji huyo alifikishwa mahakamani hapo mwishoni mwa wiki iliyopita na kusomewa shitaka la wizi wa fedha hizo, mali ya mke wa marehemu Kulola, Elizabeth Kulola ambapo wakili wa serikali, Castuce Ndamugoba, mbele ya Hakimu Mfawidhi, Angelo Rumisha alimsomea shitaka lake.
Ndamugoba aliiambia mahakama kuwa mchungaji Michael anashitakiwa kwa kosa la wizi wa fedha hizo chini ya vifungu vya 258 (i) na 265 vya sheria ya kanuni ya makosa ya adhabu, sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Alisema, huku akifahamu ni kosa na kinyume cha sheria, mshitakiwa alidaiwa kutenda kosa hilo kutoka kwenye akaunti namba 0061016209  mali ya Elizabeth Kulola katika Benki ya FMBE iliyopo Barabara ya Station.
Wakili huyo alidai mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo kati ya Septemba 20, mwaka jana na Januari 21, mwaka huu.Baada ya kusomewa mashitaka, mchungaji huyo alikana ambapo wakili wake, Deocless Rutahindurwa wa kampuni ya uwakili ya Rwelu aliiomba mahakama impe mteja wake dhamana ambayo aliambiwa ipo wazi.
Hata hivyo, Rumisha alisema kutokana na wingi wa fedha hizo, mshitakiwa atatakiwa kuweka dhamana kwa ya Sh. milioni 16.5 au wadhamini wawili wanaofahamika na wenye mali isiyohamishika.
Wadhamini hao walitimiza masharti kwa kuweka hati za nyumba, wanasubiri kesi kutajwa tena.

No comments:

Post a Comment