Sunday, May 18, 2014

Mwakapugi afariki Dunia

Dar es Salaam. Aliyekuwa Katibu Mkuu wizara ya Nishati na Madini, Arthur Mwakapugi amefariki dunia jana alipokuwa amelazwa katika Hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu ya Kansa ya Ini.
Mwakapugi ambaye amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 64, alitumikia taifa kwa miaka 30 mfululizo kabla ya kufikwa na umauti usiku wa kuamkia jana saa 3:45 ikiwa ni wiki moja tangu aliporejeshwa kutoka India kwa matibabu zaidi.
Hayo yalizungumzwa jana na msemaji wa familia, Mathias Mwambona wakati wa mazungumza na waandishi wa gazeti hili -nyumbani kwa marehemu huku akifafanua juhudi zilizofanyika bila mafanikio tangu alipoanza kusumbuliwa na ugonjwa wa kansa ya ini. Mwambona alisema marehemu Mwakapugi ambaye ameacha mjane na watoto wawili, kabla ya umauti wake alianza kusumbuliwa na ugonjwa huo miezi sita iliyopita kupitia maumivu ya tumbo yaliyomsumbua.
“Ndugu waliamua kumpeleka hospitali mbalimbali kupima bila matokeo yoyote, lakini baadaye alipimwa tena Muhimbili ambako madaktari walithibitisha kuwa na ugonjwa wa kansa ya ini,” alisema Mwambona na kuongeza:
“Mwezi huu tukaamua kumpeleka India ambako tulielezwa tayari kansa ilikuwa imeshafikia ‘stage four’(isiyoweza kutibika tena), alikaa huko akitumia huduma ya mionzi(Chemotherapy) kabla ya kumrejesha Aga Khan Jumamosi iliyopita.”
Utumishi wake serikalini
Marehemu Mwakapugi aliyeacha mjane na watoto wawili, alitumikia nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwamo Shirika la Viwango nchini(NBS), Mkurugenzi wa Tume ya Mipango 1999 mpaka 2006 kabla ya kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini tangu mwaka 2006 mpaka 2010.
Baada ya kustaafu mwaka 2010, marehemu Mwakapugu aliendelea kufanyakazi katika taasisi nyingine zinazojihusisha na masuala ya kiuchumi kupitia Taasisi ya Utafiti ya Kuondoa Umaskini(Repoa).
Mwili kuagwa leo
Katika hatua nyingine Mwambona alieleza utaratibu wa kuaagwa mwili wa marehemu leo nyumbani kwake eneo la Mikocheni B, Kinondoni jijini Dar es Salaam huku ndugu, jamaa na viongozi wakitarajiwa kushiriki katika tukio kwa ajili ya kuaga kwa mara ya mwisho.
Baada ya tukio hilo, mwili utasafirishwa kwenda kuhifadhiwa kijijini kwao Ilundo, iliyopo Wilaya ya Tukuyu mkoani Mbeya.
“Leo jioni tutaanza na ibada na kisha kuuaga mwili wa marehemu halafu kesho ndiyo tutausafirisha kwenda kijijini,” alisema Mwambona ambaye ni mjomba wa marehemu.

 Mwandosya amlilia

Akionyesha masikitiko yake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Kazi Maalumu, Profesa Mark Mwandosya alisema katika kipindi cha miaka 30 wakati wa utumishi wake, Mwakapugi alitimiza wajibu wake huku akionyesha mchango mkubwa zaidi hata baada ya kustaafu.
“Taifa lilianza kumtegemea tangu utawala wa hayati Mwalimu Julius Nyerere katika mikutano ya kimataifa, na Umoja wa Mataifa iliyohusiana na masuala ya uchumi,” alisema na kuongeza:
“Lakini hata baada ya kustaafu bado aliendelea kujihusisha na uandishi wa vitabu vya uchumi, akafanya kazi kwenye Taasisi ya Utafiti ya Kuondoa Umaskini(Repoa), lengo lake likiwa ni kuendelea kuisaidia jamii ya Watanzania.”
Mtoto wake amlilia
Katika hatua nyingine, mtoto wa marehemu Mwakapugi, Margareth Mwakapugi alionyesha hisia zake za majonzi huku akieleza kumbukumbu pekee atayoendelea kuitumia kama ngao aliyomwachiwa baba yake.

No comments:

Post a Comment