Wednesday, July 16, 2014

WEZI WAIBA KILOMITA KUMI ZA RELI


Wezi wa vyuma chakavu wameiba karibu kilomita 10 za mataruma ya reli katika njia ya reli inayofanya kazi, na kusababisha hasara ya takriban dola milioni 2.3.
Mataruma hayo yaliibwa katika reli inayopitisha treni kutoka Johannesburg kwenda katika karakana zilizopo kwenye mji wa Nigel, limeripoti gazeti la The Star. Watu watano wamefikishwa mahakamani baada ya "kukutwa kwenye eneo la tukio" na walinzi waliokuwa wakifanya doria katika reli hiyo.
"Ni wataalam, hawafanyi makosa," amesema Thumbu Mahlangu, mjumbe wa kamati ya usafiri. Msemaji wa idara ya reli Mike Asefovitz amesema: "Hawa si watu wadogo. Kuchukua uzito kama huu na kukata vyuma, unahitaji vifaa maalum." Vyuma hivyo vimeripotiwa kuwa na thamani ya dola 120,000 katika soko la vyuma chakavu.
Wizi huo umesababisha treni mpya 34 kukwama katika karakana, ambapo zilitakiwa kuanza kazi hivi karibuni, na wafanyakazi karibu 700 wapo hatarini kupoteza ajira zao. Wizi wa vyuma ni tatizo kubwa Afrika Kusini linalosababisha hasara ya kiuchumi ya mamilioni ya dola kila mwaka.


Kwa hisani ya Salim Kikeke

No comments:

Post a Comment