Tuesday, June 17, 2014

HII NDIO KAWE, JIMBO LA VIGOGO NA UTAJIRI LINALOZONGWA NA MIGOGORO LUKUKI YA ARDHI

Mbunge wa Jimbo la Kawe, Halima Mdee.

KAWE ndiyo jimbo lenye vitega uchumi vingi na vikubwa vinavyoliingizia taifa pato kubwa. Hili ni moja kati ya majimbo kadhaa ya uchaguzi jijini Dar es Salaam, likiwa na eneo kubwa la fukwe za Bahari ya Hindi lililoambaa kuanzia katikati ya jiji mpaka maeneo ya Msasani, Kawe, Kunduchi mpaka Mbweni.

 Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka.

 Kama kawaida, Gazeti la Uwazi limeingia katika mitaa mbalimbali ya kata kumi za jimbo hili tajiri lenye mahoteli mengi ya kitalii, viwanda vikubwa, ofisi za mashirika na makampuni makubwa, balozi za nchi kadhaa kubwa ikiwemo Ubalozi wa Marekani na maofisi mengi ya serikali.
Katika ziara hiyo iliyochukua siku kadhaa katika jimbo hili linaloongozwa na Mhe. Halima James Mdee kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Uwazi limebaini matatizo mengi yanayowakabili wananchi, kubwa likiwa ni migogoro sugu ya ardhi inayotishia usalama wa raia na mali zao.
MATATIZO YA WANANCHI
Ukiachilia mbali migogoro ya ardhi inayolikabili Jimbo la Kawe, ukiwepo ule mkubwa na sugu wa Kijiji cha Chasimba kilichopo katika Kata za Wazo na Bunju ambapo wananchi wa eneo hilo wanavutana na mwekezaji wa Kiwanda cha Saruji cha Twiga (Wazo Hill),
mgogoro mkubwa uliowahi kusababisha vifo vya mabaunsa wa Madale na mgogoro mwingine wa machimbo ya kokoto ya Mtongani, Kunduchi, Uwazi limebaini matatizo mengine kadhaa yanayowakabili wananchi wa jimbo hili.
Matatizo hayo ni: Ukosefu wa huduma bora za kijamii zikiwemo maji safi, hospitali na umeme, ukosefu wa ajira kwa vijana wengi na matukio ya kihalifu yanayotingisha maeneo mengi hasa katika Fukwe za Bahari ya Hindi maeneo ya Kawe, Msasani na Kunduchi.
Matatizo mengine ni ukosefu wa miundombinu bora kama barabara na madaraja, ukosefu wa vyumba vya kutosha vya madarasa, walimu wa kutosha na vifaa vya kujifunzia na kufundishia yakiwemo madawati,
uporaji wa viwanja vya wazi vilivyotengwa na serikali, ujenzi holela wa ‘mahekalu’ kwenye maeneo ya fukwe za Bahari ya Hindi, kwenye uoto asili wa mikoko, ujenzi kwenye mikondo ya maji unaosababisha mafuriko wakati wa mvua na mgogoro wa makazi na mafao kati ya waliokuwa wafanyakazi wa Kiwanda cha Tanganyika Packers kilichopo Kata ya Kawe na serikali.
MAELEZO YA MBUNGE
Baada ya kuwahoji wananchi wa maeneo mbalimbali ya jimbo hilo na kueleza matatizo yanayowakabili, Uwazi lilimsaka Mbunge Halima Mdee na kutaka kufahamu namna alivyotimiza ahadi zake alizozitoa wakati wa uchaguzi na jinsi anavyoshughulikia kero na matatizo yanayowakabili wapiga kura wake.
Jitihada za kumtafuta, ziligonga mwamba baada ya kumweleza mwandishi kwa njia ya simu kwamba alikuwa Dodoma kwenye Bunge la Bajeti ya Serikali 2014/15 na badala yake, akaelekeza kuwa majibu ya maswali yote yatatolewa na katibu wake kwa niaba yake.
Uwazi lilisaga lami hadi Magomeni Usalama kwenye ofisi za mbunge huyo na kufanikiwa kukutana na makatibu wawili kati ya watatu wa mbunge huyo, Martha Mtiko na Edward Simbeye ambao walikuwa na maelezo yafuatayo:
1. MIGOGORO YA ARDHI
Kupitia kwa makatibu wake hao, mbunge alikiri kuijua migogoro ya ardhi inayowasumbua wapiga kura wake, ukiwemo wa Kijiji cha Chasimba.
“Ni kweli kuna mgogoro mkubwa katika kijiji hicho, mwekezaji alienda mahakamani na kuwashitaki wananchi kwa madai kuwa wamevamia eneo lake, hukumu ikapita kwamba wananchi walipwe fidia na kuhamishwa lakini mheshimiwa mbunge ameendelea kuwapigania wananchi kwa nguvu zote kwani Kijiji cha Chasimba kipo pale kisheria na kilisajiliwa mwaka 1975.
“Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka anafahamu kila kitu na yeye amekuwa akichangia kwa kiasi kikubwa kuuchochea mgogoro huo kwa kutoa maamuzi yenye kutia shaka, likiwemo suala la wakazi wa eneo hilo kulipwa fidia zao ambapo mchakato mzima umeendeshwa kwa ujanjaujanja na kuibua hasira kali kwa wananchi,” alisema Mtiko kwa niaba ya Mdee.
Akizungumzia mgogoro mwingine wa mipaka kati ya wachimba kokoto, wakazi wa Mtongani (Kunduchi) na kambi ya jeshi, katibu mwingine wa mbunge, Simbeye alisema Mdee amejitahidi kulishughulikia suala hilo mpaka jeshi likaamua kurekebisha mipaka yake.
“Mpaka sasa mgogoro ule ambao ulisababisha maafa makubwa umemalizika kwa jitihada za mbunge na wananchi na wanajeshi wanaishi kwa amani isipokuwa kuna mgogoro mwingine ndani ya eneo hilohilo unakaribia kulipuka kwani manispaa inadai eneo hilo ni lake kisheria na wakati huohuo linawaachia wananchi wanaendelea kujenga, hilo nalo mheshimiwa analishughulikia,” alisema Simbeye.
2. VITENDO VYA KIHALIFU UFUKWENI
Ofisi ya mbunge ilikiri kulifahamu tatizo hilo na kueleza kwamba mbunge amejitahidi kwa kadiri ya uwezo wake kulishughulikia lakini anakwamishwa na utendaji mbovu wa jeshi la polisi kwani licha ya wananchi na mbunge kutoa taarifa mara kwa mara juu ya makundi yanayoendesha uhalifu huo hasa nyakati za jioni, wamekuwa wakishindwa kuchukua hatua za haraka.
3. HUDUMA ZA KIJAMII
“Mbunge amejitahidi sana kuboresha huduma za kijamii, ukiachilia mbali fedha za bajeti zinazotengwa na zile za mfuko wa jimbo, mheshimiwa pia amefikia hatua mpaka ya kutoa fedha zake za mfukoni ili kuboresha huduma za kijamii ikiwemo kununua madawati na vifaa vya kujifunzia na kufundishia kwa ajili ya shule mbalimbali.
“Ameshajenga zahanati kadhaa kwenye maeneo ya Salasala, Mbezi Juu, Kunduchi, Wazo na Mbopo na kusimamia ukarabati wa nyingine nyingi jimboni. Pia amefanikisha kupatikana kwa maji ya bomba katika maeneo ya IPTL (Wazo), Kawe Ukwamani, Mbweni, Makongo na kuna miradi inayoendelea maeneo ya Mabwepande, Mbuyuni na kwingineko,” alisema Mtiko.
“Pia mbunge amefanikisha kuunganishwa kwa umeme kwenye maeneo ya Mivumoni, Bunju, Salasala, Wazo Mji Mpya, Nakasangwe, Manyema na maeneo mengine,” aliongezea Simbeye.
4. TANGANYIKA PACKERS
Makatibu hao wa Mhe. Mdee waliliambia Uwazi kwamba mbunge amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha waliokuwa wafanyakazi wa kiwanda cha Tanganyika Packers waliosimamishwa kazi kuanzia April 30, 1992 kwa likizo isiyo na malipo baada ya kiwanda kufilisika, wanalipwa mafao yao.
Hata hivyo anakumbana na kikwazo kikubwa kutoka kwa serikali ambayo inabomoa nyumba za wanyonge na kuwaacha vigogo kadhaa wa serikali waliojenga ufukweni na kwenye mikondo ya maji wakipeta.” Watumishi wengi wa serikali, wanamkwamisha, makusudi ili ionekane chama cha upinzani hakiwezi kazi,” alisema Simbeye.

No comments:

Post a Comment