Monday, June 30, 2014

MTATIRO ANG'OLEWA CUF

Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba na Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad wakiondoka makao makuu ya chama hicho, Buguruni Dar es Salaam jana, baada ya kikao cha Baraza Kuu. Picha ya CUF 

Dar es Salaam. Baraza Kuu la Uongozi la Chama cha Wananchi (CUF) limemchagua Mbunge wake wa Viti Maalumu, Magdalena Sakaya kuwa naibu katibu mkuu wa chama hicho upande wa Tanzania Bara kushika nafasi iliyoachwa wazi na Julius Mtatiro.
Pia limemchagua Waziri wa Biashara wa Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui kuwa naibu katibu mkuu wa chama hicho upande wa Zanzibar nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Hamad Masoud.
Mtatiro hakuingia katika kinyang’anyiro cha kuwania nafasi hiyo kutokana na kutokuchukua fomu kugombea ujumbe wa Baraza Kuu ambayo ndiyo sifa inayotakiwa kuingia katika sekretarieti ya chama hicho.
Akizungumza jana kwa simu, Naibu Mkurugenzi wa Habari wa CUF, Abdul Kambaya alisema awali, Sakaya alikuwa akishindana na Mbunge wa Viti maalumu,
Kuluthum Mchuchuli kabla ya mpinzani wake kujitoa akisema ana imani kubwa na Sakaya ambaye aliibuka na ushindi wa kura 51 kati ya 52 zilizopigwa. Moja iliharibika.
Upande wa Zanzibar, Mazrui alimshinda Mbunge wa Viti Maalumu, Zahra Ahmed Ali baada ya kupata kura 51 na Zahra akiambulia moja.
Akizungumzia uchaguzi huo, Mtatiro alisema ana imani kubwa na Sakaya kutokana na uwezo mkubwa wa siasa alionao akisema ameking’arisha chama hicho ndani na nje ya nchi.
Alisema katika kipindi cha miaka mitatu alichoshika wadhifa huo amekuwa mkomavu katika siasa baada ya kuchota hekima za viongozi wazoefu wa kitaifa.
“Kupumzika majukumu haya makubwa ni faraja kwangu na kutanipa muda wa kutosha wa kukamilisha shahada ya tatu ya sheria,” alisema Mtatiro.
Alisema ataendelea kutumia uzoefu alioupata kukieneza chama hicho ili kuhakikisha kinaweka mizizi Tanzania Bara.
“CUF ni kila kitu kwangu bado najiona nina deni kubwa katika chama changu, leo, kesho na keshokutwa nitakuwa nafikiria nini nikifanyie chama changu na siyo chama kinifanyie nini mimi,” alisema.

No comments:

Post a Comment